Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt. John Pombe Magufuli
Raymond Mushumbusi - Dar es salaam.
Rais wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania Mhe. Dkt John Pombe Magufuli amewaagiza wakuu wa mikoa wote nchini
kusimamia ulinzi na usalama katika mikoa wanayoiongoza ili kuhakikisha suala la
amani linaendelea kuwepo na kudumishwa nchini na watu watafanya kazi kwa bidii
na hatimaye wataweza kujipatia maendeleo ya hali juu .
Akitoa agizo hilo mara
baada ya kuwaapisha wakuu wa mikoa leo Ikulu Jijini Dar es Salaam Rais wa
Jamhuri ya muungano wa Tanzania Mhe. Dkt John Pombe Magufuli amesema suala la
ulinzi na usalama wa mikoa lipo chini ya mkuu wa mkoa na hategemei kuona
matatizo ya kiusalama yanashamiri katika mikoa wakati mkuu wa mkoa husika yupo.
“Nimewaamini na
kuwapa nafasi za kuongoza mikoa, sasa basi naomba msimamie suala la ulinzi na
usalama katika mikoa yenu sitegemei kuona kwa mfano wasafiri katika mikoa ya
Kigoma au Kagera wanasindikizwa na polisi wakati wakisafiri hii itadhihirika
wazi kabisa kuwa mkuu wa mkoa umeshindwa kazi,” alisema Rais Magufuli.
“Kwanini Burundi au
Rwanda hakuna majambazi lakini nchini kwetu ndani ya mikoa yetu vitendo vya
ujambazi vimeshamiri, nawaagiza mkafanye kazi na wala msiogope mtu,
tukawatumikie wananchi wetu kwani wanatutegemea,” alisema Rais Mhe.Dkt
Magufuli.
Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Kigoma
Brigedia Jenerali Mstaafu Emmanuel Maganga amesema atatumia uzoefu alionao wa
miaka 37 katika kutekeleza agizo la Mhe. Rais
katika kusimamia masuala ya ulinzi na usalama kwa kushirikiana na
viongozi wa vyombo vya ulinzi na usalama wa mkoa huo ili kuimarisha ulinzi na
usalama kwa wananchi na mali zao.
“Nitasimamia vizuri
maagizo ya Mhe.Rais ya kusimamia suala la ulinzi na usalama katika mkoa wangu
ukizingatia tunapakana na nchi kadhaa jirani ila nitafanya kazi niliyotumwa
kuifanya ya kuwahakikishia wananchi wa Kigoma wanaishi na kufanya kazi zao za
kila siku katika usalama,” alisema Brigedia Jenerali Maganga.
Rais Magufuli
amewaapisha wakuu wa mikoa 25 kwenda kuwatumikia wanachi wa mikoa hiyo na kutatua
changamoto katika sekta mbalimbali zikiwemo sekta ya Afya,Elimu na Maji katika
kuletea maendeleo pia amewaapisha Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato ya
Tanzania(TRA) Alphayo Kidata na Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana
na Rushwa (TAKUKURU) Kamishna wa Polisi Valentino Longino Mlowola .

No comments:
Post a Comment