Trending News

CCM Adverts and Promo

Tuesday, June 21, 2016

RAIS DKT.JOHN POMBE MAGUFULI ABARIKI MAPATO YAKE YOTE KUKATWA KODI STAHIKI

RAIS John Magufuli ametuma ujumbe bungeni kuwa yeye ni mbunge namba moja na anataka mapato yake yote yakatwe kodi stahiki, hatua inayofuata ni kutoachwa kwa mtu yeyote katika suala la kodi ya mapato.
Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango alitangaza ujumbe huo wa Dk Magufuli kwamba alipewa mapema alipopeleka pendekezo la kukata kodi ya mapato katika kiinua mgongo cha wabunge. Kwa mujibu wa Dk Mpango, kabla hata ya kuwasilisha mapendekezo ya Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2016/2017, alipeleka mapendekezo hayo ya kwa Rais Magufuli.

“Nataka niwaambie, nilipopeleka hili (kukata kodi kiinua mgongo cha wabunge) kwa Rais, alinishangaa na kisha akasema yeye ni Mtanzania na ni lazima Watanzania wote walipe kodi kwa ajili ya kuendeleza nchi yao. “Rais alisema yeye ni mbunge wa kwanza wa Tanzania mpya na anapenda awe wa kwanza kukatwa kodi stahiki katika mapato yake, hivyo sasa kiinua mgongo cha Rais kitakatwa kodi,” Dk Mpango aliwaambia wabunge wenzake jana wakati akifanya majumuisho ya Bajeti ya Serikali kwa mwaka 2016/17.

Kutokana na kauli hiyo ya Rais, Dk Mpango alisema hata Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa viinua mgongo vyao lazima vikatwe kodi. Alimgeukia Naibu Spika, Dk Tulia Ackson, akamwambia kuwa na yeye lazima akatwe kodi kisha akawageukia mawaziri, akawakumbusha kuwa wao ni wabunge na kwa dhamana waliyopewa kuwa mawaziri, wanapaswa kuongoza kwa mfano katika kukatwa kodi ya mapato katika mapato yao.

Hatua hiyo, kwa mujibu wa Dk Mpango, inashuka katika ngazi zote za uongozi, kwa wakuu wa mikoa na wakuu wa wilaya, ambao nao pia kiinua mgongo chao, lazima kikatwe kodi. Akifafanua hatua hiyo ya serikali kukata kodi ya mapato kwa kila mtu, waziri alisema sheria inataka vyanzo vyote vya mapato vikatwe kodi na kiinua mgongo ni moja ya vyanzo vya mapato vinavyotambulika na sheria hiyo.

Alisema kila Mtanzania amekuwa akikatwa kodi hiyo isipokuwa wachache na hatua hiyo ya serikali inalenga kutoa haki sawa katika utozaji kodi kwa jamii yote. Baada ya muda, Naibu Spika, Dk Tulia alitania mbona Mwanasheria Mkuu George Masaju na Spika Job Ndugai hawajatajwa au wao wamesamehewa; na katika jibu la ishara, Dk Mpango alionesha kutikisa kichwa kueleza kuwa hawajasamehewa, bali nao watakatwa kodi hiyo.

Kuhusu sababu ya kuwasilisha mapendekezo hayo ya kodi wakati kiinua mgongo cha wabunge kitakatwa kodi wakati wakimaliza kipindi chao cha miaka mitano, Dk Mpango alitoa sababu mbili za hatua hiyo. Mosi, alisema anakusudia kujenga utaratibu wa kutabirika kwa mapato ya serikali, lakini pili akitokea mbunge akakoma ubunge kabla ya wakati huo, makadirio yake ya kiinua mgongo, yakatwe kodi hiyo.

No comments:

Post a Comment