Serikali ya Tanzania imeendelea kupokea maombi ya wawekezaji hususani katika miradi mbalimbali ya uzalishaji na usambazaji umeme.
Waziri
wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo amekutana na kuzungumza na
Ujumbe kutoka Kampuni ya NARI Group Corporation ambayo ni Kampuni Tanzu ya
Shirika la Gridi ya Taifa la China, ambao walimweleza Waziri kuwa, pamoja na
madhumuni mengine, wana nia ya kuzalisha umeme.
Makamu Meneja Mkuu wa
Kampuni hiyo, Bao Tianhua amemueleza Waziri Muhongo kuwa, Kampuni yake inao
mtaji wa kutosha pamoja na teknolojia ya kisasa katika uzalishaji umeme.
Aliongeza kuwa Kampuni ya NARI ina uzoefu mkubwa katika kutekeleza miradi ya
umeme kwani ilianza kufanya kazi kutoka miaka ya 1960.
Akijibu swali la
Waziri kuhusu kiwango cha umeme ambacho Kampuni yake imejipanga kuzalisha
endapo itakubaliwa maombi yake, Tianhua amesema wamejipanga kuzalisha umeme wa
kiasi cha megawati 300 hadi 400 kwa kuanzia.
Kuhusu
nia ya Kampuni yake kuwekeza katika uzalishaji wa umeme nchini, Tianhua amesema
kuwa wangependa kushirikiana na Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) katika
mradi huo ambapo NARI watawezesha masuala yote ya kiuchumi katika mradi.
Vilevile, amesema
kuwa lengo lao ni kuzalisha umeme kwa kutumia gesi kupitia teknolojia
ijulikanayo kitaalam kama ‘combined cycle’.
Akitoa mwongozo
kuhusu maombi yaliyowasilishwa, Profesa Muhongo amewataka wawekezaji hao
kukutana na kuzungumza na TANESCO pamoja na Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na
Maji (EWURA) ili kujadili kwa kina kuhusu mapendekezo husika na kwamba, iwapo
maombi yao yatakubaliwa, ndani ya kipindi cha mwezi mmoja (Aprili 15 mwaka
huu), NARI wanatakiwa wawe wamethibitisha iwapo watafanya uwekezaji huo ama la.
“Muda tunaotoa kwa
sasa si zaidi ya mwezi mmoja, hivyo ndani ya mwezi mmoja, iwapo maombi yenu
yatakuwa yamekubaliwa, mtapaswa kuwa mmewasilisha jibu lenu.”
Aidha, Waziri Muhongo
amewataka NARI kuwasilisha kwa TANESCO na EWURA mapendekezo mengine waliyowasilisha
kwake kuhusu nia ya kuwekeza katika miradi ya umeme vijijini kwa kutumia
teknolojia ya makontena maalumu pamoja na miradi ya umeme jua. Aliwataka
kuzungumzia hayo katika kikao kilichopangwa kufanyika baina yao.
No comments:
Post a Comment