Trending News

CCM Adverts and Promo

Tuesday, April 19, 2016

UZINDUZI WA DARAJA LA KIGAMBONI NA HOTUBA ALIYOITOA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA DKT.JOHN POMBE MAGUFULI.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt John Magufuli akisalimiana na baadhi ya viongozi mara baada ya kuwasili katika ufunguzi wa Daraja la Kigamboni leo
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt John Magufuli akiwasalimia wananchi waliohudhuria halfa ya uzinduzi wa daraja la Kigambini leo
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt John Magufuli akikata utepe ishara ya kulizindua rasmi daraja la Kigamboni
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt John Magufuli pamoja na viongozi wa serikali na wadau wa maendeleo wakifurahia kuzinduliwa kwa daraja la Kigamboni
Baadhi ya wananchi na wageni toka nje ya Tanzania waliohidhuria uzinduzi wa daraja la Kigamboni



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt John Magufuli akiteta jambo na aliyekuwa mkurugenzi Mkuu wa NSSF Dkt. Ramadhani Dau wakati wa uzinduzi wa daraja la Kigamboni



Na.Mwandishi Wetu - Dar- es -Salaam.




Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt.John Pombe Magufuli amezindua rasmi  daraja la Kigamboni lenye urefu wa mita 680 ambalo limegharimu kiasi cha dola za kimarekani milioni 135.0.

Akizungumza katika sherehe hizo leo jijini Dar es Salaam  Mhe.Dkt.Magufuli ameeleza kuwa fedha za mradi huo ni mapato ya ndani ambapo serikali imechangia asilimia 40 huku asilimia 60 zikiwa zimetolewa na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii NSSF.


Aidha aliongeza kuwa kupitia daraja hilo kero zilizokuwa zikiwakumba wakazi wa Kigamboni na maeneo ya jirani zitakuwa zimepungua kwa kiasi kikubwa na hivyo kuwapa unafuu katika usafiri.


“Kukamilika kwa daraja hili kwa kiasi kikubwa kumesaidia kuondoa kero waliokuwa wakikutana nazo wakazi wa Kigamboni hususani pale kivuko kinapokuwa na hitilafu  kwa sasa watakuwa na urahisi wa kupita na kuweza kufika katika maeneo yao ya kazi mapema,”alisema Mhe.Dkt.Magufuli.


Aliongeza kuwa Serikali inafanya juhudi kubwa kuhakikisha kuwa inatatua kero ya foleni katika jiji la Dar es Salaam  kwa kumaliza tatizo  hilo na ikishindikani kumaliza basi ni kulipunguza.


Mhe.Dkt.Magufuli alisema kupitia daraja hilo  uchumi wa wananchi wa Dar es Salaam  na Tanzania kwa ujumla utaongezeka kupitia  wawekezaji ambao  watawekeza  katika  maeneo ya Kigamboni pamoja na utalii wa kulitembelea daraja hususani nyakati za usiku ambapo huwa linavutia sana.


“Daraja hili ni kivutio kikubwa cha utalii ukizingatia ni daraja la kwanza kujengwa katika nchi za ukanda wa Afrika ya Mashariki na nyakati za usiku linakuwa na sura nzuri kupitia taa zilizowekwa maeneo haya” alisema Mhe.Dkt. Magufuli.


Pia alitoa wito kwa kuwaomba watanzania kuwa wazalendo kwa kulipa kodi ili serikali iweze kupata fedha za kujenga miradi mingine mingi kwa manufaa ya wananchi na hivyo kubadilisha maisha yao kupitia huduma mbalimbali.


Pia aliwasihi wananchi kuwa watu wa kuthamini na kutunza miradi inayotekelezwa na serikali kwa  kulitunza na kulithamini  daraja hilo huku kila mmoja akiwa mlinzi wa mwenzake kwa kutoa taarifa katika mamlaka husika pale anapoona uharibifu unatendeka .


 Kwa upande wake,  Naibu Waziri wa Ujenzi ,Uchukuzi na Mawasiliano Mhe.Eng.Edwin Ngonyani ameeleza kuwa kukamilika kwa ujenzi wa daraja hilo ni maendeleo makubwa kwa Dar es Salaam na nchi ya Tanzania kwa ujumla kwa kuwa utarahisisha hali ya usafiri kwa wakazi wa Kigamboni na hivyo kuvutia wawekezaji zaidi.


Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) Eng.Patrick Mfugale amebainisha kuwa ujenzi wa daraja la Kigamboni ulianza kufanyiwa usanifu tangu mwaka 1976 na 1978 lakini utekelezaji wake ulikuja  kufanyika mwaka 2012 ambapo Rais mstaafu wa awamu ya nne Mhe.Dkt.Jakaya Kikwete aliweka jiwe la msingi na hatimaye leo limezinduliwa na Rais wa awamu ya Tano Mhe.Dkt.John Pombe Magufuli.


Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Hifadhi ya Jamii  Prof.Godius Kahyarara ameeleza kuwa ujenzi wa Daraja la Kigamboni umekamilika chini ya mkandarasi  wa kampuni ya  China Railway Construction Engineering Group ikishirikiana na kampuni ya China Major Bridge Engineering.

Mapokezi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.John Pombe Magufuli akiwasili Kigamboni kuzindua daraja hilo.
Baadhi ya wananchi na wageni mbalimbali waliohudhuria ufunguzi wa daraja hilo leo
Daraja la Kigamboni kama linavyoonekana mara baada ya kukamilika.Daraja hilo lina urefu wa mita 680.
Sehemu ya majengo ya Utawala na uendeshaji wa daraja hilo





No comments:

Post a Comment