Trending News

CCM Adverts and Promo

Sunday, December 13, 2015

PONGEZI KWA RAIS MSTAAFU WA AWAMU YA NNE,DKT.JAKAYA MRISHO KIKWETE

"Jumuiya ya Wazazi CCM Mkoa wa Morogoro inapenda kutoa shukruani za dhati kwa uongozi uliotukuka na imara ulioneshwa na Rais mstaafu wa awamu ya Nne,Dkt.Jakaya Kikwete"-Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi Mkoa-Morogoro,Bi.Mecky Mdaku.

Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete. Rais mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Hongera!!

Ni vigumu kuamini kuwa kipindi cha miaka kumi ya uongozi wako ndani ya serikali umemalizika . Miaka kumi imekuwa kama siku kumi. Mengi umeyafanya kwa chama  chetu na Serikali. Hongera sana.


Rais mstaafu wa awamu ya nne-Dkt.Jakaya Kikwete


Umekiongoza chama chetu kwa mafanikio ukitumia Hekima, Busara na maarifa kuhakikisha kuwa chama chetu kinakuwa imara na kinaendelea kushika dola na kuongoza Serikali. Imani waliyoijenga watanzania kwa Chama chetu na kukipa ushindi wa kishindo katika Chaguzi zote ni kielelezo  cha uongozi wako uliotukuka. Umetuachia Chama imara na Serikali imara  yenye uwezo wa kusimamia maendeleo ya Nchi yetu.

Katika kipindi chote cha uongozi wako umehakikisha kuwa Chama na Jumuiya zake kimeendelea kuwa Imara na hususani Jumuiya ya Wazazi ambayo bila miongozo yako isingekuwa hivi ilivyo leo. Umetujengea imani ndani ya Jumuiya na ndani ya Chama na kutufanya tujisikie ni sehemu muhimu ya Chama chetu. Tutaendelea kukuenzi ndani ya Jumuiya na Chama chetu kwa ujumla.

Umoja wa Wazazi, Jumuiya ya Chama cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Morogoro kwa heshima na unyenyekevu mkubwa unapenda kukupongeza Mhe. Dr. Jakaya Mrisho Kikwete Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuliongoza Taifa letu kwa kipindi cha miaka 10.

Tunatambua ukuu na ugumu wa kazi hii kubwa kuliko zote nchini mwetu na tunazielewa changamoto nyingi ulizokumbana nazo katika kipindi chote cha miaka 10. Tunafahamu mzigo wa kutekeleza matumaini na matarajio ya kila mtanzania kwa kipindi cha miaka 10. Kwa kutambua yote haya na kwa kutambua jinsi ulivyoifanya kazi hii kwa uadilifu uzalendo na umakini wa hali ya juu, tuna kila sababu ya kukupongeza na kukushukuru kwa jinsi ulivyojitolea kulitumikia Taifa lako.

Mhe. Rais, umefanya mambo mengi katika kipindi cha uongozi wako na kwa heshima sisi Umoja wa Wazazi, Jumuiya ya CCM Mkoa wa Morogoro tunaomba tuyakumbuke na kuyataja machache kwani kwa nafasi ya makala hii pekee haitatosha kuyaeleza yote.

Mhe. Rais kwanza kabisa tunakupongeza na kukushukuru kwa kuenzi na kusimamia Amani, Umoja na Mshikamano wa Watanzania. Tunatambua kuwa hii ilikuwa ajenda yako ya kwanza na hakika tunakushukuru kwa kulinda na kuitunza tunu hii muhimu kwa Taifa letu.

Mhe. Rais, Amani na utulivu ndio msingi wa uimara wa Taifa lolote, tunatambua jinsi ambavyo umesimamia na kulinda na ushuhuda wa hili ni jinsi ambavyo umekuwa mstari wa mbele kuihubiri kwa maeneo na vitendo. Ahsante Mhe. Kikwete kwa kuiacha nchi ikiwa tulivu na salama.

Jambo la pili Mhe. Rais ni juhudi na mchango wako katika kukuza na kusimamia Demokrasia nchini mwetu. Katika kipindi cha uongozi wako tumeshuhudia demeokrasia ikipanuka na uhuru wa vyombo vya habari na watu kujieleza umepanuka zaidi., vyama vya siasa na makundi mbalimbali ya Jamii yamepata fursa ya kufanya kazi zao kwa uhuru zaidi pengine kuliko kipindi chochote tangu tupate uhuru.

Busara, hekima na utashi wako wa kutaka kila mtu asikike ndio msingi wa kukua na kuimarika na hata wenzetu wa upande wa pili ni mashuhuda wa hili japokuwa mwanadamu ameumbwa kutoridhika hawawezi kuacha kupiga kelele kwa hili pia Mhe. Rais tunaomba tukushukuru.

Jambo la tatu mhe. Rais ambalo Mtanzania yeyote muungwana hawezi kukusahau ni uimarishaji wa miundombinu hususani barabara.
Taifa letu halijawahi kushuhudia barabara bora za kiwango cha lami kwa urefu tulionao sasa. Tunafahamu kuwa, hakuna nchi inayoweza kupata maendeleo ya haraka na hata kukua kiuchumi kama hakuna miundombinu imara ya usafirishaji. Leo hii kila kona ya Tanzania inafikika kwa mchana mmoja na thamani ya mazao inaongezeka kwani kuna unyumbafu wa kutosha wa biashara ya mazao ya kilimo na biashara.

Hata wanaobeza mafanikio yako mioyoni wanasutwa na mafanikio uliyoyapata kwenye sekta ya uchukuzi, kwani kwa sasa kila mkoa umeunganishwa na barabara za lami.

Jambo la nne Mhe. Rais ni mchango wako na kujitoa kwako katika kuimarisha elimu. Umefanya mengi na kila mwenye nacho ni shuhuda, wapo wanaotamba kuna wao ndio waliojenga shule za kata na chuo kikuu cha Dodoma. Hiki ni kichekesho . Mafanikio yote haya yamekuja chini ya uongozi wako tumepata shule za kata, tumepata shule za msingi tumejenga maabara za kutosha kila shule na tumepata chuo kikuu cha Dodoma ambacho ni kikubwa kuliko chuo chochote Afrika Mashariki. Mafanikio haya si madogo  na hayakushuka kama maua jangwani bali yametokana na uongozi wako mahiri na mapenzi uliyonayo kwa nchi yako na watanzania wanzeko.

Jambo la tano ambalo Mhe. Rais tunapenda kukupongeza ni uimarishaji wa Sekta ya Afya. Tunashuhudia ukihakikisha kuwa hospitali nyingi zinapanda hadhi na kuwa hospitali za Wilaya na za Rufaa. Dhamira yako ya kusogeza huduma bora za afya karibu  na wanachi zimezaa matunda na leo tumeshuhudia upasuaji mkubwa wa moyo ukifanyika katika hospitali ya Rufaa ya Muhimbili. Tunaomba Rais ajaye ambaye tunaamini atatoka CCM, aanzie ulipoishia kwa kuendelea kusogeza huduma karibu na wanachi, kuongeza watumishi pamoja na kuhakikisha madawa yanapatikana.

Jambo la sita Mhe. Rias ni sekta ya michezo. Umefanya makubwa na yoote uliyoahidi ikiwemo kulipia gharama za wataalamu na wakufunzi umeyatimiza. Umekuwa mstari wa mbele katika kutetea haki za wasanii na hata kusaidia ukuaji wa tasnia ya sanaa na muziki, Tanzania vinajiendesha kibiashara vinaleta ajira na kuwapatia wasanii vipato vya jasho lao.

Jambo la saba Mhe. Rais ni fursa kwa wanawake. Wewe ni muhimili mkubwa wa fulsa ya “Wanawake Wanaweza” umefanya makubwa kwa kuwawezesha na kuwainua akina mama ikiwemo kuongeza idadi yao katika nyadhifa za kuchaguliwa na kuteuliwa. Leo hii tumeshuhudia akina mama wakishiriki katika ujenzi wa Taifa, wapo Mawaziri, Makatibu wakuu, Wakurugenzi, Majaji, mahakimu, Wabunge, wawakilishi na hata Spika wa bunge lililomaliza muda wake ni mwanamke. Tumekupongeza kwa ujasiri wa kuwaamini kina mama na hakika hawakukuangusha.

Jambo la nane Mhe. Rais ni mchakato wa Katiba. Ulithubutu na ukaweza kuanzisha na kusimmia mchakato wa Katiba kwa mara ya kwanza tangu awamu ya kwanza umefanya uamuzi mgumu na wa muhimu wa kuanzisha mchakato wa Katiba . Ni matumaini yetu kuwa Raisi ajaye kutoka CCM atakaribisha mchakato na kutupatia katiba bora kwa ajili ya maendelezo ya Taifa letu.

Mhe. Rais umefanya mengi lakini kama ilivyo  hapo awali tumetaja machache. Itoshe tu kusema asante sana kwa utumishi uliotukuka. Daima tutakukumbuka na kuyaenzi mafanikio yako. Tunakupongeza sana sana. Mama yetu mama Salma na familia yako kwa kukubali kukuachia uwatumikie watanaznia kwa moyo mmoja. Tunajua waliku- miss na sasa ni wakati wako wa kupumzika na kuungana na familia yako.

Mungu akujalie afya njema katika kipindi chote cha mapumziko na tunaomba uache milango wazi tuendelee kuchota burasa zako.

AHSANTE BABA KIKWETE!!!!!!




No comments:

Post a Comment